Saturday, May 23, 2015

SITAKI MIKOGO YAKO

SITAKI MIKOGO YAKO

Nachoka kuvumilia, na kwenu sifiki tena
Sakafu yenye zulia, pale kwangu mimi sina
Kile unacholilia, sitapata cha thamana
Sitaki yako mikogo, na kwetu twala mihogo.



Kwetu sisi wala tope, jikoni palala paka
Nawewe pakamapepe, nyumba kubwa umetoka
Mie kwako kijikupe, ‘meamua kuondoka
 Sitaki yako mikogo, na kwetu twala mihogo.

‘Kitaka piza kidogo, asilani huzipati
Sebeha twala mihogo, chaichapwa kwa bahati
Siendi kwenye unyago, swahibu ‘menisaliti
Sitaki yako mikogo, na kwetu twala mihogo.


Kazi yangu mshahara, ni tarehe hamsini
Ni kama sina ajira, na utani‘ta mhuni
Kunifata ni hasara, kheri nirudi nyumbani
Sitaki yako mikogo, na kwetu twala mihogo.


Mahari milioni kumi, sitapata kama poza
‘Tabidi nifyate ndimi, kisabuni ‘tajikaza
Nitaikaikanyanga lami, ninywe mchuzi wa pweza
Sitaki yako mikogo, na kwetu twala mihogo.


Bora uache mashobo, upunguze kujipenda
Wewe watafuna bibo, mimi naramba maganda
Usinione kizibo, na haja yako ni soda
Sitaki yako mikogo, na kwetu twala mihogo.


Ninafunika pazia, Kubai ninaondoka
Mahaba yamefifia, yamegeuka mzuka
Kikomo nimeshatia, nyuma sitaigeuka
Sitaki yako mikogo, na kwetu twala mihogo.


UTUNZI WA JICHO LA PEMBENI
Malenga Wa Nchi Kavu©2015

No comments:

Post a Comment